Thursday, June 7, 2012
YANGA NA SIMBA MAMA YAO NI MMOJA
Kikubwa zaidi ninachojaribu kukiangalia ni jinsi ambavyo viongozi wa vilabu vya SIMBA na YANGA wasivyopenda kufuata taratibu na kanuni zilizowekwa, mwenyekiti wa SIMBA ameongelea kwa jazba kubwa sakata la beki wa timu yake Kelvin Yondani kusajiliwa na Yanga, si ajabu kesho tu tukasikia viongozi wa YANGA nao wakilijibu hili kwa mbwembwe.
Lakini mwisho wa siku ni lazima tukubali kuwa viongozi wote hawa wa simba na yanga wana mapungufu makubwa sana katika utendaji wao wa Kazi, na namna wanavyoendesha vilabu vyao na mpira wa Tanzania kwa ujumla.
Viongozi hawa wa SIMBA na YANGA Wamekuwa wakifanya mambo mengi sana ya ajabu ajabu. SIMBA na YANGA ni vilabu ambavyo vinatakiwa kuwa mfano wa kuigwa na vilabu vingine vidogo hapa nchini.
Lakini kwa mambo ambayo yamekuwa yakifanyika ndani ya vilabu hivi vikubwa ni ya ajabu sana na ya kusikitisha mno.
Kwa sakata hili la KELVIN YONDANI kumekuwepo na watu ambao wamekuwa wakijaribu kumshutumu mchezaji huyo, lakini mimi binafsi siwezi kumshutumu hata kidogo kwanza, hatujui wakati anasainishwa mkataba na Yanga alikuwa katika mazingira gani labda alitekwa na kulazimishwa,
Pili, labda aliamua tu kusajili huku akisema liwalo na liwe hao Simba wenyewe wamenisainisha mkataba kwa 'mkopo' wakati Yanga wamekuja mezani na mipesa yote hii.
Tatu, kusukumwa na hisia za kukumbuka manyanyaso yasiyoisha ya kushutumiwa kufungisha, mara ugomvi na baadhi ya viongozi Simba.Nne, kutokutambua umuhimu na kuuheshimu mkataba wake na Simba.
Kwa nchi za wenzetu zilizoendelea kitendo cha mchezaji kusaini mkataba ni kitu muhimu mno, lakini huku kwetu umuhimu na thamani ya mkataba hujulikana wakati wa matatizo hasa pale tu mchezaji anapotaka kuondoka na kwenda kujiunga na klabu nyingine.
Mimi nina uhakika wa zaidi ya asilimia mia moja kwamba hakuna mchezaji anayechukua mkataba na kuusoma, kuuelewa vipengele vilivyomo kabla ya kuusaini.
Ninachojua ni kwamba mchezaji huwa anaangalia napata kiasi gani…nazungumza hili kwasababu nina uhakika nalo na lilishawahi kunitokea wakati nacheza mpira, wakishakubaliana anaonyeshwa pakuweka saini na dole gumba kisha anachukua mzigo wake na kusepa.
Ndio maana wenzetu huwa wanawatanguliza wawakilishi, mchezaji anapokwenda kusaini mkataba ni lazima kuwa na meneja/wakala ama mwanasheria wake, lakini hapa kwetu Tanzania ni kinyume kabisa,wachezaji wenyewe hata darasa la saba hawajamaliza halafu anaenda kusaini mkataba tena wa kisheria tena ulioandikwa kwa lugha ya kiingereza, je ana uwezo wa kuelewa? au tunadanganyana tu na kupotezeana muda.
Professionalism inatakiwa kuanzia kwa viongozi wa vilabu kabla ya wachezaji, kwa maana viongozi wanatakiwa kusimamia sheria kama zilivyo, lakini cha kustaajabisha viongozi hao hao wa vilabu ndio wanakuwa vinara kwa kupindisha sheria hizo na kushindwa kwenda nazo sambamba.
Hivyo inapotokea ishu kama hii ya leo pasipo kufuata uweledi ndipo mmoja anaonekana kuonewa au kwenda against na mwenzake lakini kumbe wote wana makosa makubwa.
Ina maana hawa viongozi wanaowasainisha hiyo mikataba ya kisheria hao wachezaji hawajui kama hawana elimu ya kutosha ya kuisoma na kuielewa hiyo mikataba jamani hii lugha ya kiingereza inayotumika kwenye hii mikataba (mimi mwenyewe inaniacha ) ni mchezaji gani wa kitanzania mwenye uwezo wa kuisoma na kuielewa kabla ya kusaini na kuweka dole gumba? kama kweli hawa viongozi wanawatakia mema hawa wachezaji kwanini hiyo mikataba isiwekwe kwenye lugha ya Kiswahili angalau wanaweza kuambulia kitu. ( au kisheria ni lazima mkataba uwe kwenye lugha ya kiingereza ?)
Ishu kama hii ya YONDANI bila kuhangaika sana ebu tuangalie KANUNI ZA USAJILI zinasemaje
Kanuni ya 57
Uhamisho wa mchezaji
(1) Kilabu inaweza kumhamisha mchezaji kutoka kilabu kimoja hadi kingine, kwa madhumuni ya kumsajili, baada ya ligi kumalizika, au katika kipindi cha usajili wa katikati ya msimu. Kilabu inayotaka kumsajili mchezaji aliyesajiliwa na kilabu kingine au mwenye mkataba na kilabu kingine, italazimika kuafikiana na kilabu yake kabla ya kumsajili mchezaji huyo. Hata hivyo kilabu ambayo itaruhusiwa kusajili mchezaji katikati ya msimu ni ile ambayo haijatimiza wachezaji thelathini (30) au ile ambayo imempa mchezaji wake ITC ya kwenda kucheza soka nje ya nchi, au ile ambayo mchezaji wake amehamia kilabu kingine cha ndani kwa mujibu wa kanuni hii.
Kanuni ya 45
Usajili na uhamisho wa wachezaji
(4) Mchezaji ana uhuru wa kujisajili na kilabu kingine katika msimu mmoja iwapo kutakuwa na maelewano kati ya kilabu yake na ile inayotaka kumsajili.
(5) Kilabu inawajibika kuingia mkataba na mchezaji wa kuichezea lakini mkataba huo ni lazima uthibitishwe na TFF. Ada ya kuthibitisha mkataba ni shilingi elfu hamsini (50,000/=).
(6) Mchezaji ambaye ameingia mkataba wa zaidi ya msimu mmoja hatoruhusiwa kujisajili na kilabu kingine kabla ya kilabu yake mpya kuafikiana na kilabu yake ya zamani.
Kanuni ya 56
Katazo
Haitaruhusiwa kwa mchezaji yeyote kutia saini kwenye mikataba wa vilabu viwili tofauti kwa wakati mmoja na inayohusu kipindi kimoja. Mchezaji atakayesaini mikataba ya timu mbili tofauti kwa wakati mmoja, ataadhibiwa kwa mujibu wa kanuni ya 44 (4) ya kanuni hizi.
Kutokana na vipengele hivyo hapo juu hakuna mchezaji ambaye anaweza kuhama timu moja kwenda timu nyingine kihuni huni tu pasipo kufuata kanuni na taratibu.
Sakata la Simba na Azam juu ya usajili wa Ibrahim Jeba.
Lazima tusiwe wanafiki, waswalihi wanasema mkuki kwa nguruwe ila kwa binadamu mchungu, wakati tukiwa tunalijadili sakata hili la Yondani si vibaya pia tukaliwe mezani sakata linalomuhusu mchezaji Ibrahim Jeba aliyesajiliwa na Simba Kutoka Azam pasipo taratibu kufuatwa.
Kanuni ya 44
Masharti ya mikataba kati ya wachezaji na kilabu
(1) Muda wa chini wa mkataba utakuwa kuanzia tarehe ya kuanza kutumika hadi mwisho wa msimu. Muda wa juu wa mkataba utakuwa ni kipindi cha miaka mitano (5). Mikataba ya muda mwingine wowote itakubaliwa kama inafuata Sheria ya Mikataba inavyosema. Mchezaji chini ya umri wa miaka 18 haruhusiwi kuingia kwenye mkataba wa mchezaji wa kulipwa kwa kipindi kinachozidi miaka mitatu (3), sharti lolote linalotaja kipindi kirefu zaidi halitatambuliwa.
(2) Kilabu inayotarajia kuingia mkataba na mchezaji wa kulipwa haina budi kuiarifu kilabu yake ya sasa kwa maandishi kabla ya kufanya makubaliano na mchezaji huyo wa kulipwa. Mchezaji wa kulipwa atakuwa huru tu kuingia mkataba na kilabu nyingine iwapo mkataba wake na kilabu yake ya sasa umekwisha au utakwisha baada ya miezi sita (6). Uvunjaji wowote wa sharti hili utastahili vikwazo vinavyofaa.
Niliposema viongozi wote hasa wa vilabu vya SIMBA na YANGA ndo wenye matatizo makubwa nilikua namaanisha vitendo kama hivi.
Kufanya mazungumzo ya siri na mchezaji pasipo kupata ruhusa ya klabu yake ni kosa kubwa ambalo hata FIFA wanalipiga vita.
Ina maana Kulwa na Doto hawazijui hizi taratibu na kanuni za kusajili mchezaji ?
Labels:
By Elicy Michael
Location:
Mwanza, Tanzania
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment